Saturday 31 May 2014

MIMBA ZA UTOTONI, KIKWAZO KWA WASICHANA MBEYA, PWANI NA MARA

WAKATI imebakia miaka miwili kuhakikisha malengo ya milenia yanatekelezwa, baadhi ya watoto wa kike nchini Tanzania, wamekuwa wakifukuzwa shule kutokana na ujauzito, huku wengine wakiacha wenyewe masomo pale tu wanapojigundua ni wajawazito.

Maeneo ambayo ymebainika kuwepo kwa hatari hiyo inayoendelea kwa watoto hao wa kike ni wilayani Ileje, Kyela mkoani Mbeya, Musoma mkoani Mara na Bagamoyo mkoani Pwani.



Msichana Mwanaharusi Mkupi (17) mkazi wa kijiji cha Yombo wilayani Bagamoyo mkoani Pwani, ambaye anasema kuwa alikuwa na ndoto ya kuwa Daktari,  ni mmoja kati ya wasichana waliokatisha masomo yao kutokana na ujauzito alioupata akiwa darasa la tano.

Anasema alirubuniwa na mvulana ambaye ni dereva wa pikipiki ,akajiingiza kwenye mahusiano ya ‘’ki-ngono’’ akapata ujauzito  na kukatisha masomo ya elimu ya msingi.

Mama yake Mwanaharusi aliyejitambulisha kwa jina la Habiba Bakari (45) anasema, alijua kama binti yake amepevuka lakini  hakuwahi kumfundisha  masuala ya afya ya uzazi kwani alikuwa akisubiri ahitimu darasa la saba ili amuweke ndani, kwa ajili ya kumpa mafunzo  ya namna ya kujihadhari na wanaume, lakini  akapatwa na mshtuko baada ya kumuona mwanae ni mjamzito.

‘’Mila zetu  mtoto wa kike anapopevuka hulazimika kukaa ndani bila kuonekana na watu wengine ambao si wanafamilia, kwa muda wa mwezi mmoja au zaidi, akifundishwa jinsi ya kujitunza na kujiepusha na vitendo vya ngono’’ anasema Habiba.

Anasema kutokana na utaratibu  uliowekwa na kijiji cha Yombo ni kwamba mtoto afanyiwe mafunzo hayo baada ya kumaliza darasa la saba, basi hata yeye alikuwa akisubiri muda huo ufike, “nadhani kuna kitu nilitakiwa kufanya lakini kwa sasa nimechelewa” anasikikitika.

Wakati mama yake  Mwanaharusi akijilaumu kwa kushindwa kumfundisha mwanae namna ya kujikinga na ujauzito, Pili Amada  (17) naye amejikuta akipata ujauzito akiwa na umri wa miaka 16, hali ambayo anaijutia kwani hana biashara yoyote inayomwingizia kipato na kujikuta akimtegemea mama yake kwa malezi ya mwanae.

Anasema alipata ujauzito akiwa tayari amepata mafunzo ya kimila, lakini anaweka wazi kwamba alipokuwa ndani alikokuwa akifundishwa, aliambiwa kwamba  ameshapevuka hivyo akikutana na mwanaume atapata ujauzito.

Anatanabaisha  kuwa licha ya kuambiwa hivyo, hakuwahi kuambiwa kuhusu namna ya kujikinga ndipo akajiingiza  kwenye vitendo vya ngono na kupata ujauzito.

Anasema anajisikia vibaya  kumuona mama yake ambaye ni mkulima, akihangaika kutafuta mahitaji yake pamoja na mwanae kazi ambayo angetakiwa kuifanya yeye na mwenza wake aliyempa ujauzito. 

Anasema hana namna nyingine ya kufanya kwani tangu mwanaume alipompa ujauzito hajawahi kupeleka matunzo ya mtoto.

Pili ambaye alipata ujauzito baada tu ya kumaliza darasa la saba, anasema akiwa shuleni hakuwahi kufundishwa njia za  kujikinga na ujauzito,  zaidi ya kuambiwa mabadiliko ambayo atayapata atakapopevuka lakini hiyo haikuwa kinga ya kushinda vishawishi vya wanaume.

Mganga mkuu wa zahanati ya Yombo, Donald Malamsha anasema wasichana wa kijiji hicho hasa wanafunzi wa shule ya msingi, wanaogopa kufika zahanati  kupata ushauri wa namna ya kujikinga na ujauzito kwa kile alichokiita “kuona aibu” kwamba wataonekana  wanajihusisha na vitendo vya ngono wakiwa bado wadogo.

‘’Wasichana wengi  hufika katika hapa kupata ushauri wa kutumia njia za uzazi wa mpango, wakiwa tayari na watoto’’ anasema Mganga huyo.

Malamsha, anasema athari zinazoweza kujitokeza kwa wasichana ambao hawajafikisha umri wa miaka 18 wanapopata ujauzito, anasema mara nyingi huvuja damu nyingi wakati wa kujifungua.

Anasema upo uwezekano mkubwa wa kuzaa mtoto ambaye hajafikisha miezi tisa tumboni (njiti), pia  mtoto atakayezaliwa, anaweza  kupata utindio wa ubongo na msichana kupata uzazi pingamizi na hatimaye kufanyiwa upasuaji wakati wa kujifungua.

Mwalimu  mkuu wa shule ya msingi Yombo, Ostina Gama anakiri kwamba katika shule yake wanafunzi wengi wa kike wanakatisha  masomo kutokana na kupata mimba.

Anasema wakati somo la sayansi  lenye mada za uzazi  likifundishwa  darasa la saba na darasa la sita, baadhi ya  wanafunzi  hupata ujauzito wakiwa darasa la nne na darasa la tano kabla hawajapata elimu hiyo.

Diwani wa kata ya Yombo, Idd Mazongela, anakiri kuwepo kwa tatizo la mimba za utotoni katika kata yake, anasema kwa sasa anaomba mashirika na taasisi binafsi zinazotoa elimu ya afya ya uzazi shuleni, kutembelea kata yake kwani anaamini elimu ya afya ya uzazi ikifundishwa kikamilifu basi tatizo la mimba za utotoni litaondoka.

Anasema wanafunzi wanaopata ujauzito mara nyingi hurubuniwa na vijana wenzao, hali inayoonyesha kukosekana kwa elimu ya afya ya uzazi kwa jinsia zote yaani vijana wa kike na wa kiume.

Afisa elimu wa wilaya ya Bagamoyo, Juma Kabelwa, anasema kwa sasa tatizo la mimba za utotoni limepungua kidogo katika wilaya hiyo ikilinganishwa na miaka ya nyuma.

Anasema kwa mwaka jana 2012, ni mwanafunzi mmoja tu kwa wale waliojiandikisha kufanya mtihani wa darasa la saba  katika wilaya nzima ambaye alikutwa na ujauzito.

Takwimu za wizara ya elimu na mafunzo ya ufundi za mwaka 2010,  zinaonyesha kuwa wanafunzi 500 walikatisha masomo katika mkoa wa Pwani pekee,  kati ya mwaka 2005 na 2009 kutokana na ujauzito.

Kwa upande wa wilaya ya Kyela mkoani Mbeya, nako hali hiyo ya watoto wa kike kupata ujauzito wakiwa bado hawajafikisha umri wa miaka 18, unaotambulika kikatiba kuwa  mtu mzima.

Josephine Boazi (17) mkazi wa kijiji cha masoko kata ya Busale wilayani Kyela, alikatisha masomo yake akiwa kidato cha kwanza kutokana na kupata ujauzito.

Anasema hakuwahi kufundishwa namna ya kujikinga na ujauzito, kwa sasa yupo nyumbani akiwategemea wazazi wake katika kumlea mwanae na yeye pia.

Mama yake Josephina, aliyejitambulisha kwa jina la Stella Mbukwa, anasema si jambo la kawaida kwa mama kuzungumzia masuala ya uzazi kwa binti yake kwani ni kitu ambacho hakipo katika mila na desturi zao.


Wakati Stella akiona aibu kuzungumza na binti yake, tamko la serikali  kuhusu  uzazi wa mpango kwa vijana , linasema  vijana wote wana haki ya kupata taarifa, elimu na ushauri nasaha kuhusu njia za uzazi wa mpango, tamko ambalo Stella anakiri kuwa hajawahi kuliona wala kulisikia.

Katika wilaya ya Ileje mkoani Mbeya, nako kuna idadi kubwa ya wanafunzi wanaoacha masomo kutokana na mimba za utoto ambazo baadhi zinaambatana na maambukizi ya virusi vya Ukimwi(VVU).

Mkurugenzi wa shirika lisilokuwa la kiserikali la Hossana Ows Centre la wilayani humo linaloshughulika na masuala ya afya, Nsanya Mwalyego, anasema kuwa mpaka sasa shirika lake linahudumia zaidi ya wananchi 350 ambao wanaishi na maambukizi ya virusi vya ukimwi.

Anasema idadi hiyo ni ya wananchi waliopo katika kata nne tu kati ya kata kumi na nane zilizopo katika wilaya hiyo ya ileje.

‘’Tuanahudumia watu 350 waliojitokeza katika kata nne ambazo ni Itumba, Isongole, Chitete na Mlale tu ambao tunawafundisha jinsi ya kujikinga na maambukizi mapya, kutojinyanyapaa na tunawapatia dawa baridi kwa wagonjwa wa majumbani wakiwemo wenye vidonda’’ alisema Mwalyego.

Kaimu mratibu wa kitengo cha Ukimwi mkoa wa Mbeya Dr.Francis Philly, anasema kuwa mwitikio wa wagonjwa wanaotumia dawa za ARV kuwa ni mkubwa kwani takwimu zinaonesha kuwa kuanzia June 2004 hadi June 2012 wagonjwa waliojiandikisha katika huduma ni 106598 ambapo watu wazima ni 92085 na watoto ni 12889.

Kwa mujibu wa sera ya taifa ya afya ya uzazi ya mwaka 2007, inasema uzazi wa mpango ni haki ya kimsingi ya kila mtu, bila kujali kama ameolewa au kuoa na kama amezaa au hajazaa.

Wakati sera ikisisitiza kuwa uzazi wa mpango ni haki ya kila mtu, Pili Makuri (18) mkazi wa kijiji cha Bweri, wilaya ya Musoma mkoani Mara, anasema alipata ujauzito akiwa darasa la tano na akiwa na umri wa miaka 16 alizaa kwa upasuaji, kutokana na nyonga yake kuwa ndogo, kulingana na umri wake  mdogo.

Lakini mtoto akiwa na mwaka mmoja akapata ujauzito mwingine ambao ulimfanya afanyiwe tena upasuaji,. anakiri kwamba  hali hiyo imetokana na kutokufahamu njia za kuzuia  ujauzito usiotarajiwa.

Ripoti ya wizara ya afya na ustawi wa jamii ya mwaka 2011 inaonyesha  kwamba, asilimia 25 ya wanawake walio katika umri wa kuzaa ambao wangependa kupumzika, kupangilia uzazi,  hawatumii njia yoyote za uzazi wa mpango.

Utafiti wa Shirika la afya Duniani (WHO) na (UNFPA), kuhusu masuala ya mimba za utotoni, unaonyesha  kuwa  wasichana milioni 14 mpaka 15 ambao wako chini ya umri  wa miaka 18 wanakuwa tayari wana watoto  kwa kila mwaka, hii ikionyesha kuwa ni sawa na asilimia 10  ya  uzazi  kwa dunia nzima.

Malengo ya Milenia yaliyotamkwa na nchi  193 wanachama wa Umoja wa Mataifa (UN) mwaka 2005 mjini New York Marekani, yamelega kuhakikisha kuwa ifikapo mwaka 2015,  watoto wote wa kiume na wa kike  waweze kumaliza masomo yao ya  elimu ya msingi.

Uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa makala haya mkoani Mbeya, Pwani na mkoani Mara katika wilaya za Ileje, Kyela, Bagamoyo, Bunda, Butiama na Musoma, umebaini kuwa watu wengi wanaotumia mipira ya kiume (Kondomu), huwa wanatumia siku ya kwanza mpaka ya tatu na baada ya hapo hawatumii kabisa na baadhi wanapokutana na wanafunzi wa kike huwa hawatumii hata siku ya kwanza.

Mwandishi wa makala haya anapatikana kwa simu 0754 440749, barua pepe; kalulunga2006@gmail.com

No comments:

Post a Comment